Tanzania emblem
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

OFISI YA WAZIRI MKUU

Habari

Dkt. Yonazi atoa pole kwa waathirika wa maafa Moshi


Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge na Uratibu Dkt. Jim Yonazi ametoa salamu za pole kwa familia zilizopata msiba wa ndugu wanne wa familia ya moja ya Marehemu Edward Chaki waliofariki kwa kuangukiwa na nyumba kutokana na maporomoko ya udongo na mawe kutoka katika milima inayozunguka nyumba kadhaa katika kata ya Kimochi Kijiji cha Lyakombila Wilaya ya Moshi Vijijini Mkoani Kilimanjaro yaliyosababishwa na mvua zinazoendelea kunyesha nchini.

Dkt. Yonazi amefika katika maeneo hayo kutembela nyumba hizo pamoja na kuzungumza na wakazi hao ikiwa ni sehemu ya ziara yake ya kikazi ya kujionea hali halisi ya madhara yatokanayo na mvua zinazoendela kunyesha katika maeneo mbalimbali ya nchini.

Akiwa katika ziara hiyo, alitembelea maeneo mbalimbali ikiwemo; makazi yaliyoathiriwa na mvua hizo, miundombinu ya barabara pamoja na madaraja,maeneo yaliyojirani na Mto Rau ambapo aliongozana na timu kutoka Ofisi yake kutoka Idara ya Menejimenti ya Maafa, baadhi ya watendaji kutoka Ofisi ya Mkuu wa Mkoa huo, Viongozi wa Wilaya ya Moshi pamoja na ujumbe kutoka Bonde la Mto Pangani.

Aidha alitumia fursa hiyo kuwapa pole wafiwa wote huku akiendelea kutoa rai kwa kila mwananchi kuwa mstari wa mbele katika masuala ya maafa kwa kuzingatia madhara  yatokanayo na maafa ikiwemo uharibifu wa miundombinu, mazao pamoja na vifo.

“Serikali inatoa pole kwa familia hii iliyofikwa na msiba mzito wa kuondokewa na baba, mtoto, kaka pamoja na mjukuu ambapo walianguikiwa na maporomoko kutoka katika milima na kupelekea umauti, hili ni pigo na tunatoa pole, Mungu aendelee kufariji familia na sisi tupo pamoja nanyi katika wakati huu wa majonzi,” alisema Dkt. Yonazi

Sambamba na hilo Dkt. Yonazi amezitembelea Kambi maalum ikiwemo ya Lucy Lameck na kambi ya shule ya msingi Ghona zilizotengwa kwa lengo la kutoa huduma muhimu kwa waathirika wa maafa hayo ikiwemo wa kata ya Saranga na Mji Mpya huku akiwasihi kuendelea kuwa watulivu na kuiunga mkono Serikali katika hatua zote za masuala ya mejenimenti ya maafa.

Awali akitoa neno la utangulizi Mkuu wa Wilaya ya Moshi Mhe. Zephania Sumaye amesema, Serikali imeendelea na hatua mbalimbali za kusaidia waliopatwa na madhara ya maafa ya mafuriko ikiwemo kuwahudumia katika kambi zilizotengwa, kutoa elimu ya taadhari za mvua zinazoendelea kunyesha na kuwahimiza wananchi kuendelea kuchukua tahadhari na kuhama maeneo hatarishi lengo ni kuwa na jamii salama na stahimilivu dhidi ya maafa na kuendelea na shughuli za uzalishaji ili kujiletea maendeleo yao na Taifa kwa ujumla.

=MWISHO=