Habari
Katibu Mkuu Dkt.Yonazi apokelewa rasmi Ofisi ya Waziri Mkuu aomba ushirikiano.
KATIBU Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu) Dkt. Jim Yonazi amepokelewa rasmi katika Ofisi ya Waziri Mkuu hii leo Februari 28, 2023 Jijini Dodoma na kutoa wito kwa Menejimenti na watumishi wa ofisi hiyo kuendelea kutoa ushirikiano katika utekelezaji wa majukumu kwa lengo la kuleta ufanisi.
Dkt. Yonazi amewasihi watumishi hao kufanya kazi kwa juhudi, upendo na Amani ili kuwatumikia wananchi na kuifaya Ofisi ya Waziri Mkuu kuendelea na jukumu lake kubwa la kuratibu shughuli za Serikali kwa matokeo chanya.
Katika hafla hiyo ya mapokezi amewasihi watumishi kuwa wamoja na kufanya kazi kwa weledi zaidi huku akiwashukuru kwa mapokezi mazuri.
Nimshukuru Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuniteua kuitumikia nafasi hii, ikumbukwe kuwa tuna jukumu kubwa la kuwatumikia wananchi hivyo tufanye kazi kwa juhudi huku tukidumisha ushirikiano, Alieleza Dkt. Yonazi.
=MWISHO=