Tanzania emblem
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

OFISI YA WAZIRI MKUU

Habari

Waziri Mkuu atoa wito kwa taasisi za kifedha kuzitambua hati za kimila


Waziri Mkuu Kassim Majaliwa ametoa wito kwa  taasisi za fedha nchini kuzitambua hati za kimila kama dhamana ya kutoa mikopo kwa wananchi.

Amesema kuwa hati zote zinazotolewa na Wizara au za kimila zinatambulika kisheria na zina fursa kwa mwenye hati hiyo kupata mikopo kutoka kwenye Taasisi za kifedha.

Ametoa wito huo Bungeni leo (Alhamisi, Mei 30, 2024) wakati akijibu swali la Mbunge wa Busokelo, Atupele Mwakibete kwenye kipindi cha maswali ya papo kwa papo kwa Waziri Mkuu ambaye alitaka kujua ni lini Serikali itabadili Sheria ya Ardhi ili watu wa vijijini watumie hati za kimila kupata mikopo.

Ameongeza kuwa inawezekana zipo taasisi za kifedha ambazo hazikubali hati hizo kwasababu ya matakwa au mpango kazi wao, lakini kwa mujibu wa Sheria hati hizo ni halali na zinatolewa kisheria kwa vipindi kama ilivyo zile zinazotolewa na Wizara kwa miaka 33, 66 hata 99

“Nitoe wito kwa Taasisi zote za kifedha ambazo zimeridhiwa na Serikali kufanya shughuli zake nchini kwa mujibu wa Sheria za nchi ziendelee kutumia na kutoa fursa kwa wenye hati za kimila au zinazotolewa na Wizara ya Ardhi kuwa ni hati halali zinatambulika na zinatoa fursa kwa mtanzania anayemiliki ardhi nchini kupata mkopo”

Katika hatua nyingine, Mheshimiwa Majaliwa amesema kuwa Serikali inaendelea na mpango mkakati wa ujenzi wa vituo vya ukaguzi katika maeneo ya Vigwaza, Dumila, Manyoni na Nyakanazi lengo ni kuimarisha usalama wa nchi, ukusanyaji wa mapato na kuondoa usumbufu kwa wasafirishaji kwa kukaguliwa kila mahali kwa kuwa vinajengwa kwa umbali ambao hauwezi kuleta usumbufu.

Kadhalika, Mheshimiwa Majaliwa amesema Serikali inaendelea na mpango wa kuziimarisha bandari za Mtwara, Tanga na ujenzi wa bandari ya Bagamoyo sambamba na kuhamasisha mataifa ya nje kutumia Bandari ya Dar es Salaam “Hii itasaidia nchi nyingi kutumia bandari zetu ambayo itasadia kuimarisha ukusanyaji wa mapato”

Amesema hayo wakati akijibu swali la mbunge wa Biharamulo Magharibi Mhandisi Ezra Chiwelesa ambaye  aliyetaka kujua mpango wa Serikali wa kukamilisha ujenzi wa  vituo vya ukaguzi katika maeneo ya Vigwaza, Dumila, Manyoni na Nyakanazi.

Pia, Mheshimiwa Majaliwa amesema kuwa Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuweka mazingira wezeshi ya uwekezaji nchini “Ninatoa wito kwa wawekezaji ambao wapo tayari kuja kuwekeza nchini kwamba Serikali yetu imefungua milango na imetoa fursa kwa wawekezaji wakubwa wa miradi ya kimkakati ikiwemo kupata punguzo kwenye maeneo kadhaa na hata urahisi katika upataji wa maeneo ya uwekezaji”