Tanzania emblem
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

OFISI YA WAZIRI MKUU

Habari

Majaliwa aipa tano Fountain Gate kutwaa ubingwa Afrika Kusini


WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa ameipongeza timu ya Mpira wa Miguu ya Wasichana ya Fountain Gate kwa kutwaa ubingwa wa Soka la Wanawake kwa Shule za Sekondari barani Afrika (CAF African School Football Championship) yaliyofanyika Afrika Kusini.

Mheshimiwa Majaliwa amesema ushindi wa timu hiyo ni heshima kwa Taifa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan ambaye amedhamiria kukuza na kuendeleza sekta michezo nchini.

Amesema hayo leo Alhamisi, (Aprili 13, 2023) alipokutana nao ili kuwapongeza kwa kutwaa ubingwa huo baada ya kuzifunga shule kutoka nchi za Gambia, Afrika Kusini, Congo na Morocco.

Waziri Mkuu amesema kuwa Rais Dkt. Samia amekuwa na utaratibu wa kufanya kukutana na timu zinazoshiriki katika michuano mbalimbali ya kimataifa lengo likiwa ni kutoa hamasa na kutekeleza azma yake ya kuimarisha sekta ya michezo nchini

Akizungumza katika tukio hilo, Mheshimiwa Majaliwa ametoa wito kwa wamiliki wa shule binafsi waanzishe idara za michezo kwenye shule zao ili kutoa fursa kwa vijana kuonesha vipaji kwa kushiriki katika michezo mbalimbali kwani itasaidia kutoa mchango kwenye Taifa kupitia sekta ya michezo.

Kwa upande wake, Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Balozi Dkt. Pindi Chana amesema kabla ya timu hiyo kwenda Afrika Kusini kushiriki michuano hiyo, tayari ilishakuwa bingwa wa mashindano kwa upande wa CECAFA kwenye mashindano kama hayo.

Naye,  Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (TAMISEMI) Angela Kairuki amewapongeza wanafunzi hao kwa kuiwakilisha vema nchi kwenye michuano hiyo iliyoandaliwa kwa mara ya kwanza. "Wasichana wakiamua jambo lolote wanaweza, yapo mengi ambayo mnaweza kuyafikia"

Mbali ya kutwaa ubingwa huo, timu ya Fountain Gate pia ilitwaa tuzo tatu zikiwemo za golikipa bora, mchezaji bora na mfungaji bora wa mashindano hayo.