Tanzania emblem
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

OFISI YA WAZIRI MKUU

Habari

Kanisa la Waadventista wa Sabato lakabidhi Tsh. Milioni 22 kwa waathirika wa maafa Hanang


Kanisa la Waadventista wa Sabato kutoka Jimbo Kuu la Kaskazini Mwa Tanzania limekabidhi msaada ya fedha zaidi ya shilingi milioni 22 za Kitanzania kwa ajili ya kusaidia waathirika wa Maafa ya Maporomoko ya tope na mawe kutoka mlima Hanang mkoani Manyara tarehe 3 Disemba, 2023.

Akizungumza tarehe 11 Disemba, 2023 wakati wa kukabidhi msaada huo Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu la Kaskazini Mwa Tanzania wa kanisa hilo Mchungaji Mark Malekana amesema kanisa linatoa pole kwa waathirika wote na wataendelea kuwaombea kwani jamii hiyo inahitaji misaada mbalimbali ikiwemo ya kiroho ili waendelee kurejea katika hali zao za awali.

“Kanisa limeguswa sana na maafa haya, na tunaungana na Serikali kwa kutoa pole na kwa leo tumekabidhi shilingi milioni ishirini na mbili na laki tano ambazo zitasaidia kuendelea kurejesha hali kwa wenzetu waliofikwa na maafa haya,”alisema Askofu Malekana

Alitumia nafasi hiyo Kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa namna alivyolisimamia suala hilo na kulipa uzito unaotakiwa kwa kuhakikisha viongozi wa Serikali wanaratibu na kushughulikia kwa ufanisi mkubwa ili kuwapa unafuu waliofikwa na maafa hayo.

“Serikali mmefanya kazi kubwa na mnaifanya usiku na mchana, Kanisa limeona liungane nanyi ikiwa ni sehemu ndogo tu, tunaahidi kuendelea kufanya zaidi kadiri Mungu anavyotubariki ili kuwapa faraja na nguvu ndugu zetu waliopata maafa,”alieleza

Akizungumza mara baada ya kupokea msaada huo Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Sera, Bunge na Uratibu Dkt. Jim Yonazi amewashukuru kwa namna walivyojitoa kifedha na kiroho huku akiahidi kuwa fedha zote zinazotolewa zitawafikia walengwa na kutumika kwa matumizi yaliyokusudiwa.

“Kanisa la Waadiventista wa Sabato tunawashukuru kwa kuendelea kutuombea naamini kwa namna mlivyojitoa leo ni jambo la baraka sana kwao na familia zao kwa ujumla kwa kuzingatia wamewapoteza wapendwa wao, niwaombe msiache kuwaombea kila siku ili Mungu aendelee kuwapa amani na furaha katika wakati wanaopitia,” alisema Dkt. Yonazi.

=MWISHO=