|
WAZIRI Mkuu Mizengo Pinda amesema uamuzi wa kurejesha michezo mashuleni siyo kwa shule za Sekondari tu bali kuanzia za msingi hadi Vyuo vya Elimu ya Juu.
Alikuwa akifungua mashindano ya Umoja wa Michezo ya Shule za Sekondari (UMISSETA) kwenye Kituo cha Elimu cha Kibaha, mjini Kibaha, mkoani Pwani leo (Jumapili, Juni 20, 2010).
“Maelekezo ya Rais Kikwete ya kurejesha michezo mashuleni ni kwa shule zote na vyuo, ili kuendeleza vipaji vya vijana katika michezo na elimu nchini,” alisema.
Waziri Mkuu pia alielekeza kuwa michezo hiyo iwashirikishe pia wanafunzi wenye ulemavu wa viungo kwa kuwa nao wanaihitaji na wanaweza kucheza michezo mbalimbali.
Alitaka pia shule zote ziwe na viwanja vya michezo na kwamba Halmashauri za Miji, Manispaa na Vijiji zihakikishe kuwa maeneo yaliyotengwa kwa michezo yanatumika kwa shughuli hiyo tu na yanatunzwa na kuendelezwa.
Mhe. Pinda aliyashukuru makampuni yaliyochangia vifaa kwa UMISSETA na kuyataka mengi yafanye hivyo kwa kuwa yatakuwa yanatimiza wajibu wao wa kuisaidia jamii (corporate responsibility).
Kanda 12 za mikoa mbalimbali nchini zinashiriki katika michezo hiyo, ikiwa ni pamoja na kanda moja ya mikoa mitano iliyoko Unguja na Pemba.
Michezo inayoshindaniwa ni Mpira wa Miguu kwa wanaume na wanawake, Mpira wa Mikono, Mpira wa Meza, Mpira wa Kikapu na Riadha.
Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Prof. Jumanne Maghembe alisema kwa sasa michezo imerejeshwa shuleni kwa kuanzia na Sekondari, lakini baadaye itarejea kote.
Michezo mashuleni ilikuwepo tangu zamani lakini katika miongo ya hivi karibuni iliondolewa na baadaye zikatolewa lawama kuwa kuondolewa huko ndiyo chimbuko la kudorora kwa vipaji vya michezo nchini.
(mwisho) |