Home | News | Waziri Mkuu alaani mauaji ya watoto Mbeya
News
Speeches

Hotuba ya Shukrani kwa Wabunge kabla ya Mkutano wa Ishirini wa Bunge la Jamhuri ya Muungano Kuvunjwa na Mheshimiwa Rais, Ukumbi wa Bunge, Dodoma, 15 Julai 2010...

Hotuba ya Mheshimiwa Mizengo P. Pinda (Mb) Waziri Mkuu Wakati wa Kufungua Kongamano la Vijana wa Vyuo Vikuu vya Dodoma katika Ukumbi wa African Dreams – Dodoma, tarehe 25 Juni 2010...

More Speeches
Recently Documents

kk Quotes

kama Bunge, lakini mmoja mmoja kama watumishi wa umma, tunao wajibu mkubwa sana wa kuishi na kutenda kwa mfano. Tujiepushe na tamaa zinazoweza kuliingizia Taifa hili hasara kubwa.

Kauli ya Waziri Mkuu kuhitimisha mjadala wa Richmond,
Mkutano wa 18 wa Bunge, Februari 10, 2010
More Quotes
Videos
Photo Gallery

Waziri Mkuu, Mizengo Pinda akiwa katika picha ya pamoja na maaskofu wa kanisa katoliki baada ya ibada ya kumsimika askofu wa jimbo la Moshi,Isaac Amani Massawe iliyofanyika kwenye kanisa kuu la Moshi mjini jan
More Photos
Documents and Publications


mgPrint friendly version mg Email this page

Waziri Mkuu alaani mauaji ya watoto Mbeya

Dodoma,17 April 2010

 
WAZIRI MKUU Mizengo Pinda amelaani vikali mauaji ya kiajabu ya watoto wadogo yaliyozuka hivi karibuni katika Tarafa ya Tukuyu Wilayani Rungwe mkoani Mbeya na kuahidi kuwa Serikali itachukua hatua kali kwa wahusika watakaopatikana na hatia.
 
Alikuwa akihutubia wazazi, walimu na wanafunzi baada ya kupokea maandamano ya watoto kuipongeza Serikali na Bunge kwa kupitisha Sheria ya Mtoto ya Mwaka 2009, kwenye Uwanja wa Jamhuri mjini Dodoma leo asubuhi (Jumamosi, Aprili 17, 2010).
 
“Inasikitisha kuona kuwa watoto hao wadogo wanauawa ovyo kikatili katika namna ya kutisha huku watu wazima wapo na wanashindwa kuwalinda,” alisema.
 
Mhe. Pinda alikumbusha kuwa matukio haya ya kuua watoto wadogo yanatokea baada ya wimbi la kuwaua walemavu wa ngozi, ambao nao wengi wao wanaowindwa ni watoto wadogo pia.
 
“Kila nikikaa sielewi. Watanzania tufike mahali kweli turejee na kusema matendo haya siyo ya kibinadamu, hayampendezi Mungu, hasa kuwaua watoto wadogo,” alisema.
 
Watoto wapatao sita wameuawa kikatili huko Tukuyu hivi karibuni na Polisi imewakamata watu kadhaa wakishukiwa kuhusika na mauaji hayo ambayo yanahusishwa na imani za kichawi.
 
Katika hotuba yake, Waziri Mkuu alisisitiza kuwa Serikali itahakikisha kwamba Sheria ya Mtoto ya Mwaka 2009 inatekelezwa kudhibiti maovu mengi yanayotendwa dhidi ya watoto. “Napenda kutoa tahadhari kwamba kuanzia sasa tunapoanza utekelezaji wa Sheria hii, yeyote atakayebainika kuendeleza vitendo viovu kwa watoto atakuwa amegusa mboni ya jicho la Serikali.”
 
“Adhabu kali itatolewa kwa yeyote atakayehusika na ukatili wa aina yoyote dhidi ya watoto. Kwa wale waliojenga mazoea ya kuwaonea watoto sasa waache mara moja, kwa sababu Sheria hii sasa itachukua mkondo wake,” alisema.
 
Sheria ya Mtoto ya mwaka 2009, inayozingatia upatikanaji wa haki za msingi za watoto na kuendeleza ustawi wao, inachukua nafasi ya Sheria tano ambazo zilifutwa na nyingine tano zilizofanyiwa marekebisho. Inaweka bayana kuwa mtoto ni yule mwenye umri wa miaka 18 na kurudi chini.
 
Ilipitishwa na Bunge katika mkutano wa 17 Novemba mwaka jana na kuanza kufanya kazi rasmi Aprili mosi, mwaka huu baada ya kutiwa saini na Rais Jakaya Kikwete.
 
Kumekuwa na lawama nchini kuwa watoto wamekuwa wakinyimwa haki zao za msingi zikiwemo za kuishi, kupata elimu, kuendelezwa, kulindwa na kutunzwa.
 
Maandamano hayo yaliwashirikisha zaidi ya watoto 27,000 wa shule za Msingi na Sekondari wa Dodoma, kuwawakilisha watoto wenzao nchini kote.
                   
 
(mwisho) 
 
 
Help | Disclaimer | Privacy | Site Feedback
Copyrights ©2008-2010, The United Republic of Tanzania, Prime Minister All Rights Reserved
Designed and published by DataVision International (T) Ltd