|
UONGOZI wa mkoa wa Dodoma umeiomba Serikali iangalie uwezekano wa kukipandisha hadhi Chuo cha Ualimu cha Mpwapwa ili kiwe Chuo Kishiriki cha Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) kama njia ya kuharakisha kupunguza tatizo la uhaba wa walimu nchini.
Ombi hilo lilitolewa jana jioni (Jumamosi, Februari 6, 2010) mjini Mpwapwa wakati wa maadhimisho ya miaka 33 ya kuzaliwa kwa CCM yaliyofanyika kimkoa wilayani humo.
Akitoa salamu za chama hicho, Katibu wa CCM mkoa wa Dodoma, Kapteni (Mst.) John Barongo alisema Chuo cha Ualimu Mpwapwa kimekuwepo nchini kwa muda mrefu na kina sifa ya kutoa mafunzo kwa walimu.
Alisema ili kuziba pengo la walimu waliobobea kwenye fani hiyo, wanaiomba Serikali ikipandishe hadhi chuo hicho ili kiwe chuo kishiriki cha UDOM.
Chuo cha Ualimu Mpwapwa ambacho kilianzishwa tangu mwaka 1892 chini ya utawala wa Mjerumani wakati huo kikiendeshwa mjini Tanga na kutoa mafunzo katika fani za elimu, kilimo, ufundi na maarifa ya nyumbani.
Mwaka 1920 kilihamishiwa Dar es Salaam wakati wa utawala wa Waingereza na mwaka 1925 kilihamishiwa Central Province na kujengwa Mpwapwa ambapo kipo hadi sasa.
Chuo hicho kina jumla ya wanachuo 1,452, ambao kati yao 688 ni wasichana na 767 ni wavulana. Pia kina watumishi 107 kati yao 57 wakiwa ni wakufunzi wenye shahada za uzamili (2), shahada za kwanza (39) na stashahada 16. Walimu wa shule ya mazoezi ni 29 na watumishi wasio wakufunzi ni 21.
(mwisho) |