| Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, amesema kuwa maridhiano yaliyofikiwa baina ya Katibu Mkuu wa Chama Cha Wananchi (CUF), Seif Shariff Hamad, na Rais wa Zanzibar, Aman Abeid Karume, yatawasilishwa na kujadiliwa kwenye Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ndipo Serikali itatoa msimamo wake.
Ametoa kauli hiyo leo asubuhi (Alhamisi, Januari 28, 2010) wakati akijibu swali na Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni, Hamad Rashid Mohamed, kwenye kipindi cha maswali ya papo kwa hapo kwa Waziri Mkuu.
Kiongozi huyo wa Kambi ya Upinzani ambaye pia ni Mbunge wa Wawi (CUF), alitaka kujua kama Serikali imeyatambua rasmi kutambua maridhiano hayo na nini msimamo wake.
Waziri Mkuu alisema anaamini katika Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) kuna mfumo mzuri wa kushughulikia masuala mbalimbali ikiwemo hilo la maridhiano ya Rais Karume na Seif.
“Ni matumaini yangu kuwa ndani ya SMZ jambo hili litaweza kujadiliwa vizuri na hatua itakayofuata ni kulileta ndani ya NEC ili nayo iweze kuielekeza Serikali ifanye nini… baada ya hatua hiyo, nitaweza kueleza Serikali imeamua nini ila kwa maoni yangu binafsi natamani pia kusikia Zanzibar ina amani,” alisema.
Katika swali lale la nyongeza, Hamad Rashid alitaka kujua kama maneno yaliyotolewa na Rais Jakaya Kikwete baada ya maridhiano hayo, yalikuwa msimamo wa Serikali.
Akijibu swali hilo, Waziri Mkuu alisema ni nia ya Serikali kuona kuwa Wazanzibari wanakuwa na amani na kwamba Rais Kikwete pia anatamani hali hiyo.
Novemba 5, mwaka jana, Maalim Seif alitangaza kumtambua rasmi Rais Karume kama Rais wa Zanzibar, kauli ambayo imeashiria kama njia ya kumaliza mpasuko wa kisiasa visiwani humo uliodumu tangu kufanyika kwa uchaguzi kwa kwanza chini ya mfumo wa vyama vingi vya siasa mwaka 1995.
|