|
* Awateua wengine wapya watano kujaza nafasi zao
WAZIRI MKUU Mizengo Pinda amewavua madaraka viongozi na watendaji wakuu wa Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo kwa kutowajibika ipasavyo na kutozingatia kanuni za fedha na kuwateua wengine wapya kujaza nafasi zao.
Waliovuliwa madaraka ni Mkurugenzi Mtendaji Bibi Rhoda Nsemwa; Mweka Hazina, Bw. Karol M. Wage; Ofisa Kilimo, Mifugo na Ushirika, Bw. Naftal Rhemtullah; Ofisa Mipango, Bw. Aloyce Gabriel na Mkaguzi wa Ndani, Bw. Abdul Mwinyi.
Mhe. Pinda alitangaza uamuzi huo mjini Bagamoyo leo (Jumatano Januari 20, 2010) kwenye mkutano na viongozi na watendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo, akiwa Waziri mwenye dhamana ya Serikali za Mitaa.
Amewavua madaraka watendaji wakuu hao wa Halmashauri ya Wilaya kwa kutumia kanuni ya 37 ya Kanuni za Utumishi wa Umma za Mwaka 2003 na kusema hatua nyingine za kinidhamu zitafuatia kadri itakavyoonekana inastahili.
Aliowateua kushika nafasi hizo ni Bw. Samuel Saiyanga kuwa Mkurugenzi Mtendaji mpya wa Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo, akitokea Halmashauri ya Wilaya ya Kigoma na Bw. Fidelis R. Nenetwa kuwa Mweka Hazina, akitokea Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga.
Wengine wapya Bagamoyo ni Fidelica Gabriel Myovelo, kuwa Ofisa Kilimo, Mifugo na Ushirika akitokea Halmashauri ya Wilaya ya Iringa; Felista Chuki Masamba kuwa Mkaguzi wa Ndani akitokea Halmashauri ya Wilaya ya Lindi na Prudence Mtiganzi kuwa Mhandisi wa Maji akitokea Halmashauri ya Wilaya ya Kilombero.
Alisema uamuzi wa kuwapumzsiha watendaji wakuu hao wa Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo unatokana na mapendekezo ya ripoti ya uchunguzi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali, Septemba na Oktoba mwaka jana.
Uchunguzi wa Mdhibiti unafuatia tuhuma za ukiukwaji wa kanuni za fedha, uzembe wa kufuatilia utekelezaji wa miradi na ubadhirifu Halmashauri hiyo.
Ripoti hiyo imebainisha ukiukwaji mkubwa wa kanuni za fedha, uzembe na kushindwa kuwajibika na matokeo yake kuzorota kwa miradi mbalimbali ya maendeleo katika Wilaya hiyo.
Waziri Mkuu alisema kuwa pamoja na kuwa hatua hizo zimechukuliwa kwa Bagamoyo, Halmashauri nyingine nchini zikae chonjo na zitashughulikiwa kwa kuwa nazo zina matatizo yanayofanana na ya Bagamoyo.
Katika ziara yake ya siku moja ya Bagamoyo leo (Jumatano, Januari 20, 2010) Waziri Mkuu pia alikagua mradi wa kilimo cha umwagiliaji cha miwa na mahindi unaoendeshwa na kampuni binafsi ya SEKAB.
(mwisho) |