|
WAZIRI MKUU Mizengo Pinda amekabidhiwa ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kuhusu tuhuma za ukusanyaji wa ovyo na ubadhirifu wa mapato ya Kituo cha Mabasi cha Ubungo jijini Dar es Salaam.
Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali, Bw. Ludovick Utouh, alikabidhi ripoti hiyo kwa Mhe. Pinda kwenye ukumbi wa Ofisi ya Waziri Mkuu majengo ya Bunge mjini Dodoma leo mchana (Jumanne, Julai 28, 2009).
Akikabidhi ripoti hiyo, Bw. Utouh alisema Ofisi yake inakamilisha pia ripoti nyingine ya uchunguzi aliouagiza Waziri Mkuu kuhusu makusanyo ya mapato ya Soko Kuu la Kariakoo, jijini Dar es Salaam.
“Hiyo ya Kariakoo tunaikamilisha, na itakuwa tayari kukabidhiwa ifikapo Agosti 15 au kabla ya hapo,” alisema Bw. Utouh.
Waziri Mkuu aliagiza ufanywe uchunguzi (Perfomance Audit) na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kuhusu mapato na matumizi ya makusanyo ya Kituo cha Mabasi cha Ubungo na Soko la Kariakoo ili kuboresha mapato ya Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam.
Mhe. Pinda alitoa maagizo hayo alipokuwa akiwahutubia viongozi mbalimbali wa mkoa wa Dar es Salaam katika majumuisho ya ziara yake ya siku nne ya mkoa huo Machi 15, 2009 kwenye ukumbi wa Diamond Jubilee.
Katika ziara yake hiyo ya kukagua usafi na mazingira ya Jiji, Waziri Mkuu alibaini pamoja na mambo mengine, Kituo cha Mabasi cha Ubungo na Soko Kuu la Kariakoo ni maeneo mawili ambayo yangeingiza mapato makubwa kwa Jiji lakini ukusanyaji wake ni wa hovyo na kuna tuhuma za ubadhirifu.
(mwisho)
|